Unyenyekevu Na Ukuu Wa Kristo

Ikiwa mmepata faraja kwa kuwa mmeunganishwa na Kristo, kama mmevutwa na upendo wake na kushiriki Roho wake, kama mnaoneana huruma na kusaidiana; basi kamilisheni furaha yangu kwa kuwa na nia moja, upendo mmoja na kuwa wamoja katika roho na shabaha. Msifanye jambo lo lote kwa ajili ya ubinafsi au kwa kujiona, bali kuweni wanyenyekevu, mkiwahesabu wengine kuwa bora kuliko ninyi. Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu ajishughulishe pia kwa faida ya wengine. Muwe na nia kama ile aliyokuwa nayo Kristo Yesu; yeye kwa asili alikuwa sawa na Mungu, lakini hakuona kwamba kuwa sawa na Mungu ni kitu cha kush ikilia sana. Bali alikubali kuacha vyote, akachukua hali ya mtumishi, akazaliwa na umbo la wanadamu. Alipochukua umbo la mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii mpaka kufa, tena kifo cha msalaba. Kwa sababu hiyo, Mungu alimwinua juu kabisa, akampa jina ambalo ni kuu kuliko majina yote; 10 ili kwa jina la Yesu, kila goti lipigwe, mbinguni na duniani na kuzimu; 11 na kila ulimi ukiri kwamba Yesu Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu

Ng’aeni Kama Nyota

12 Basi rafiki zangu wapendwa, kama ambavyo mmekuwa mkitii nilipokuwa nanyi, nawasihi mwendelee kunitii vivyo hivyo, na hata zaidi sasa kwa kuwa sipo pamoja nanyi. Endeleeni kufanya bidii kwa ajili ya wokovu wenu huku mkitetemeka na kuogopa. 13 Kwa maana ni Mungu ambaye anatenda kazi ndani yenu, akiwapa nia ya kutimiza mapenzi yake na kuwawezesha kutenda yale yanayompendeza 14 Fanyeni mambo yote bila manung’uniko au mabishano 15 ili msiwe na lawama au kosa bali muwe wana wa Mungu wasio na kasoro katika ulimwengu uliopotoka, mking’aa kama nyota angani, 16 na kusisitiza neno la uzima. Mkifanya hivyo siku ya Kristo nitajisi fia kwamba sikupiga mbio au kufanya kazi bure. 17 Hata kama damu yangu itamwagwa kama sadaka juu ya dhabihu na huduma inayotokana na imani yenu, mimi ninafurahi na kushangilia pamoja nanyi nyote. 18 Vivyo hivyo, nanyi pia mnapaswa kufurahi na kushangilia pamoja nami.

Safari Ya Timotheo Na Epafrodita

19 Nina matumaini katika Bwana Yesu ya kumtuma Timotheo hivi karibuni aje kwenu, ili nipate habari za kunitia moyo kutoka kwenu. 20 Sina mtu mwingine hapa kama yeye, anayewatakieni mema kwa moyo wote. 21 Wengine wanajishughulisha zaidi na mambo yao wenyewe na hawajali lo lote kuhusu kazi ya Yesu Kristo. 22 Lakini ninyi wenyewe mnajua jinsi Timotheo alivyojithibit isha, kwa maana amefanya kazi ya Injili pamoja nami kama vile mtoto na baba yake. 23 Kwa hiyo, natumaini kumtuma Timotheo kwenu mara tu nipatapo habari kuhusu mambo yangu yatakavyokuwa. 24 Nami naamini katika Bwana kwamba mimi mwenyewe nitakuja kwenu hivi karibuni.

25 Nimeona vema kumrudisha ndugu yangu Epafrodita kwenu. Yeye ni mtumishi na askari mwenzangu, ambaye pia ni mjumbe wenu mliyemtuma anihudumie katika mahitaji yangu. 26 Yeye ana hamu kuwaoneni ninyi nyote, na amesikitishwa kwa sababu mlipata habari kwamba alikuwa mgonjwa. 27 Hakika alikuwa mgonjwa, tena karibu ya kufa. Lakini Mungu alimhurumia, na si yeye tu, bali hata na mimi alinihurumia, nisipatwe na huzuni juu ya huzuni . 28 Kwa hiyo napenda kumtuma kwenu ili mtakapomwona kwa mara nyingine, mpate kufurahi, na mimi nipunguziwe wasiwasi wangu. 29 Kwa hiyo mpokeeni katika Bwana kwa furaha kubwa; na wapeni heshima watu kama hawa. 30 Kwa maana alikaribia kufa kwa ajili ya kazi ya Kristo; alihatarisha maisha yake ili aweze kunipa msaada ambao ninyi msingeweza kunipa.

Iweni katika Umoja na Msaidiane

Fikirini kuhusu kile ambacho tulichonacho kwa sababu tunamilikiwa na Kristo: hamasa aliyotuletea, faraja ya upendo wake, ushirika katika Roho wake, huruma na wema aliotuonyesha. Ikiwa mnazifurahia baraka hizi, basi fanyeni yale yatakayoikamilisha furaha yangu: iweni na nia moja na mpendane ninyi kwa ninyi. Iweni na umoja katika malengo yenu na katika kufikiri kwenu. Msiruhusu ubinafsi au kiburi viwe dira yenu. Badala yake muwe wanyenyekevu mkiwathamini wengine kuliko ninyi wenyewe. Kila mmoja wenu asijishugulishe kwa mema yake yeye mwenyewe bali kwa mema ya wengine.

Hivi ndivyo mnapaswa kufikiri, kuhisi na kutenda katika maisha yenu kwa pamoja, kama vile Kristo Yesu alivyofikiri:

Alikuwa sawa na Mungu katika namna zote,
    lakini hakufikiri kwamba kuwa sawa na Mungu
    kilikuwa kitu cha manufaa kwake.
Badala yake, aliacha kila kitu,
    hata sehemu yake pamoja na Mungu.
Akakubali kuwa kama mtumwa,
    akiwa katika umbo la binadamu.
Wakati wa maisha yake kama mtu,
    Alijinyenyekeza na akawa mtiifu kabisa kwa Mungu,
    hata jambo hilo liliposababisha kifo chake msalabani.
Hivyo ndiyo sababu Mungu alimpa mahali pa heshima sana,
    na akampa jina lililo kuu kuliko majina yote.
10 Hivyo kila mtu atasujudu kumheshimu Yesu.
    Kila mmoja aliye mbinguni, duniani na wale walio chini ya dunia.
11 Wote watakiri kwamba, “Yesu Kristo ni Bwana,”
    na hili litamtukuza Mungu Baba.

Iweni Kama Mungu Anavyotaka

12 Rafiki zangu wapendwa, daima mnatii yale mliyofundishwa. Kama mlivyotii nilipokuwa pamoja nanyi, ni muhimu zaidi na zaidi kwamba mtii wakati huu ambapo sipo pamoja nanyi. Hivyo ni lazima mwendelee kuishi katika namna inayoleta maana kwa wokovu wenu. Fanyeni hivi kwa wingi wa heshima na utii kwa Mungu. 13 Ndiyo, Mungu ndiye anayetenda kazi ndani na miongoni mwenu. Anawasaidia ninyi kutaka kutenda yanayomfurahisha, naye anawapa nguvu ya kuyatenda.

14 Fanyeni mambo yote pasipo kulalamika wala kubishana. 15 Nanyi mtakuwa watoto wa Mungu wasiolaumiwa na wasio na hatia. Ijapokuwa mnaishi mkiwa mmezungukwa na watu wasio waaminifu wasiojali thamani haki. Katikati ya watu hao mnang'ara kama mianga katika ulimwengu wenye giza, 16 nanyi mnawapa mafundisho yanayotoa uhai. Hivyo nitaona fahari juu yenu wakati Kristo atakapokuja tena. Ninyi ndiyo mtakaothibitisha kuwa kazi niliyoifanya haikukosa matokeo, ya kwamba nilishindana mbio na nikashinda.

17 Imani yenu inayatoa maisha yenu kama sadaka katika kumtumikia Mungu. Hata kama ni kweli kwamba sasa ninajimimina mimi mwenyewe kama sadaka ya kinywaji pamoja na sadaka yenu, ninayo furaha, na nitawashirikisha ninyi nyote furaha yangu. 18 Ninyi pia mnapaswa kufurahi na kunishirikisha furaha yenu.

Habari Kuhusu Timotheo na Epafrodito

19 Kwa baraka za Bwana Yesu, ninategemea kuwa nitamtuma Timotheo kwenu hivi karibuni. Naye atarejesha kwangu taarifa kuhusu ninyi ili nifurahi. 20 Sina mtu mwingine yeyote kama Timotheo, ambaye kwa dhati kabisa anayajali mambo yanayowahusu. 21 Wengine wote wanajishughulisha na maisha yao wenyewe. Hawajali kazi ya Yesu Kristo. 22 Mnafahamu Timotheo amejithibitisha kuwa ni mtu wa aina gani. Ametumika pamoja nami katika kuhubiri Habari Njema kwa njia ambavyo mwana angemtumikia baba yake. 23 Ninategemea kumtuma aje kwenu haraka baada ya kujua yatakayonipata. 24 Bwana hunifanya niwe jasiri ili niweze pia kuja kwenu haraka.

25 Kwa sasa, nadhani ni lazima nimrudishe Epafrodito kwenu. Ni mtumishi na mtenda kazi pamoja nami na askari mwenzangu katika jeshi la Bwana. Nilipotaka msaada, mlimtuma kwangu. Kama mjumbe wenu, alinihudumia mahitaji yangu. 26 Lakini sasa anataka kuwaona ninyi nyote tena. Ana wasiwasi sana kwa sababu mlisikia kuwa alikuwa mgonjwa. 27 Alikuwa mgonjwa karibu ya kufa. Lakini Mungu alimsaidia yeye na mimi ili nisiwe na huzuni zaidi. 28 Hivyo ninataka sana kumtuma kwenu. Ili mtakapomwona, mfurahi. Nami nitaacha kuwa na wasiwasi juu yenu. 29 Mkaribisheni kwa furaha nyingi katika Bwana. Waheshimuni watu kama Epafrodito. 30 Anapaswa kuheshimiwa kwa sababu alikaribia kufa akifanya kazi kwa ajili ya Kristo. Aliyaweka maisha yake katika hatari ili aweze kunisaidia. Ni msaada ambao msingeweza kunisaidia.